Jeremiah 3

Israeli Asiye Mwaminifu


1 a“Kama mtu akimpa talaka mkewe,
naye akamwacha na akaolewa na mtu mwingine,
je, huyo mume aweza kumrudia tena?
Je, hiyo nchi haitanajisika kabisa?
Lakini umeishi kama kahaba na wapenzi wengi:
je, sasa utanirudia tena?”
asema Bwana.

2 b“Inua macho utazame miinuko iliyo kame na uone.
Je, pana mahali ambapo hawajalala nawe?
Uliketi kando ya barabara ukiwasubiri wapenzi,
ukakaa kama yeye ahamahamaye jangwani.
Umeinajisi nchi
kwa ukahaba wako na uovu wako.

3 cKwa hiyo mvua imezuiliwa,
nazo mvua za vuli hazikunyesha.
Hata hivyo, una uso usio na haya kama wa kahaba;
unakataa kutahayari kwa aibu.

4 dJe, wewe hujaniita hivi punde tu:
‘Baba yangu, rafiki yangu tangu ujana wangu,

5 eje, utakasirika siku zote?
Je, ghadhabu yako itaendelea milele?’
Hivi ndivyo unavyozungumza,
lakini unafanya maovu yote uwezayo.”

Wito Kwa Ajili Ya Toba

6 fWakati wa utawala wa Mfalme Yosia, Bwana aliniambia, “Umeona kile Israeli asiye mwaminifu amekifanya? Amepanda juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti uliotanda na amefanya uzinzi huko. 7 gMimi nilifikiri kuwa baada ya kuyafanya yote haya angelinirudia, lakini hakurudi, naye dada yake Yuda mdanganyifu aliona hili. 8 hNilimpa Israeli asiye mwaminifu hati yake ya talaka, na kumfukuza kwa ajili ya uzinzi wake wote. Hata hivyo nikaona kuwa Yuda dada yake mdanganyifu hakuogopa. Yeye pia alitoka na kufanya uzinzi. 9 iKwa sababu uasherati wa Israeli haukuwa kitu kwake, Yuda aliinajisi nchi kwa kuzini na mawe na miti. 10 jPamoja na hayo yote, Yuda dada yake mdanganyifu hakunirudia kwa moyo wake wote, bali kwa kujifanya tu,” asema Bwana.

11 k Bwana akaniambia, “Israeli asiye mwaminifu ana haki kuliko Yuda mdanganyifu. 12 lNenda, ukatangaze ujumbe huu kuelekea kaskazini: “ ‘Rudi, Israeli usiye mwaminifu,’ asema Bwana,
‘sitakutazama tena kwa uso uliokunjamana,
kwa kuwa mimi ni mwenye huruma,’ asema Bwana,
‘Sitashika hasira yangu milele.

13 mUngama dhambi zako tu:
kwamba umemwasi Bwana Mwenyezi Mungu wako,
umetapanya wema wako kwa miungu ya kigeni
chini ya kila mti unaotanda,
nawe hukunitii mimi,’ ”
asema Bwana.

14 n“Rudini, enyi watu msio waaminifu, kwa kuwa mimi ni mume wenu,” asema Bwana. “Nitawachagua ninyi, mmoja kutoka kwenye mji, na wawili kutoka kwenye ukoo, nami nitawaleta Sayuni. 15 oKisha nitawapeni wachungaji wanipendezao moyo wangu, ambao watawaongoza kwa maarifa na ufahamu. 16 pKatika siku hizo, idadi yenu itakapokuwa imeongezeka sana katika nchi, watu hawatasema tena, ‘Sanduku la Agano la Bwana,’ ” asema Bwana. “Halitaingia tena kwenye mawazo yao wala kukumbukwa, hawatalihitaji wala halitatengenezwa jingine. 17 qWakati huo, wataita Yerusalemu kuwa Kiti cha Enzi cha Bwana, nayo mataifa yote watakusanyika Yerusalemu kuliheshimu jina la Bwana. Hawatafuata tena ukaidi wa mioyo yao miovu. 18 rKatika siku hizo, nyumba ya Yuda itaungana na nyumba ya Israeli, wao kwa pamoja watakuja kutoka nchi ya kaskazini hadi nchi niliyowapa baba zenu kama urithi.

19 s“Mimi mwenyewe nilisema, “ ‘Tazama jinsi nitakavyowatunza kwa furaha kama wana
na kuwapa nchi nzuri,
urithi ulio mzuri kuliko wa taifa jingine lolote.’
Nilidhani mngeniita ‘Baba,’
na msingegeuka, mkaacha kunifuata.

20 Lakini kama mwanamke asiye mwaminifu kwa mumewe,
vivyo hivyo mmekosa uaminifu kwangu pia, ee nyumba ya Israeli,”
asema Bwana.


21 tKilio kinasikika juu ya miinuko iliyo kame,
kulia na kuomboleza kwa watu wa Israeli,
kwa sababu wamepotoka katika njia zao
na wamemsahau Bwana Mwenyezi Mungu wao.


22 u“Rudini, enyi watu msio waaminifu,
nami nitawaponya ukengeufu wenu.”

“Naam, tutakuja kwako,
kwa maana wewe ni Bwana Mwenyezi Mungu wetu.

23 vHakika zile ghasia za kuabudu sanamu kwenye vilima
na milimani ni udanganyifu;
hakika katika Bwana, Mungu wetu,
uko wokovu wa Israeli.

24 wTangu ujana wetu miungu ya aibu imeyala
matunda ya kazi za baba zetu:
makundi yao ya kondoo na ng’ombe,
wana wao na binti zao.

25 xSisi na tulale chini katika aibu yetu,
na fedheha yetu itufunike.
Tumetenda dhambi dhidi ya Bwana Mwenyezi Mungu wetu,
sisi na mababa zetu;
tangu ujana wetu hadi leo
hatukumtii Bwana Mwenyezi Mungu wetu.”
Copyright information for SwhKC